ZURA YAFANYA UKAGUZI WA UMEME MKOA WA KUSINI

ZURA YAFANYA UKAGUZI WA UMEME MKOA WA KUSINI

Mamlaka ya Udhibiti ya Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) imefanya ukaguzi wa ubora wa huduma ya Umeme kwa kukagua Transfoma za usambazaji wa Umeme majumbani katika Mkoa wa kusini Unguja.

Mamlaka imefanya ukaguzi huo tarehe 13 Septemba 2023 kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) katika maeneo mbali mbali ikiwemo Muyuni, Kizimkazi, Jendele na Makunduchi.

Ukaguzi huo umelenga zaidi katika kuhakikisha Transfoma za Umeme zinakuwa katika mazingira salama pamoja na kuhakikisha alama za tahadhari zimebandikwa katika Transfoma hizo.

Mamlaka imependezwa na juhudi zilizochukuliwa na shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) kwa utekelezaji na uboreshaji wa Miundombinu hiyo itakayosaidia upatikanaji wa huduma ya umeme kwa kuzingatia usalama kwa watumiaji.

Mamlaka hufanya ukaguzi wa miundombinu ya Umeme mara kwa mara kwa lengo la kuimarisha huduma ya Umeme ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza katika Transfoma hizo kwa Visiwa vya Unguja na Pemba.